Rais Samia Suluhu Hassan amesema Tanzania na Kenya zimefanikiwa kuondoa jumla ya vikwazo 46 vya biashara kati ya 64 vilivyokuwepo.
Hayo yamejiri leo Desemba 10, 2021 katika mazungumzo maalumu yaliyofanyika ikulu kati ya Rais Samia Suluhu Hassan na Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta.
"Tulipokutana tulikuwa na vikwazo vingi vya biashara lakini tukasema kwa kutumia majina yetu la kwake Uhuru tukasema sasa ni uhuru wa kufanya biashara Kenya au Tanzania na la kwangu suluhu tukasema sasa tutafute suluhu ya changamoto zinazotukabili".
Katika mazungumzo hayo baadhi ya makubaliano waliyoafikiana ni pamoja na kushirikiana katika sekta ya utalii na kuwataka Mawaziri wazungumze juu ya changamoto zilizopo ili nchi zote mbili zifaidike kuleta watalii wengi.
Katika kuimarisha uhusiano kwenye masuala ya utalii wa nchi hizo Rais Samia anasema Kenya wana ndege wachache aina ya Korongo ambao wapo Tanzania hivyo waliomba ndege hao wakae kwenye mbuga zao.
"Leo hii nina furaha kumkabidhi Mheshimiwa Rais cheti maalumu cha ndege hawa 20 kuwapeleka Kenya wakae katika mbuga za wenzetu, hii ndio zawadi yetu ya Krismasi Kenya lakini na mimi nikamwambia kwenye mbuga zangu nina madume wawili tu wa faru hawana wake, sisi tupo tayari kutoa mahari"- Alisema Rais Samia.
Rais Kenyatta alifika nchini mapema jana katika maadhimisho ya sikukuu ya Uhuru wa miaka 60 ya Tanganyika yaliyofanyika jijini Dar es Salaam ambapo Rais Samia alimtambulisha kama mgeni rasmi maadhimisho hayo na kusema kuwa atafanya ziara maalum hapa nchini.