Tanzania imeadhimisha miaka 60 ya uhuru tangu ilipojinasua kutoka katika utawala wa kikoloni.
Sherehe za Maadhimisho hayo ya Miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara zimefanyika katika uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam leo tarehe 9 Desemba, 2021.
Mgeni Rasmi wa maadhimisho haya ambaye ametambulishwa na Rais Samia Suluhu Hassan ni Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi na pia anatarajiwa kufanya ziara maalum hapa nchini.
Wageni wakuu wengine waliohudhuria sherehe hiyo ni pamoja na Rais Paul Kagame wa Rwanda, Filipe Nyusi wa Msumbiji, Mwenyekiti wa AU, Rais wa DRC Felix Tshisekedi, Rais wa Comoro Azali Assoumani na Rais wa zamani wa Malawi Joyce Banda. Wengine ni wawakilishi waliotumwa na mataifa yao.
Aidha, Desmba 08 kuamkia Desemba 09, kulifanyika mkesha wa kuamkia sherehe hii ya kitaifa, Ambapo Rais Samia alihutubia taifa na kutaja mafanikio mbalimbali yaliyopatikana tangu Tanzania ilipopata uhuru na pia alieleza matumaini yake kwa zaidi, miaka ijayo.
Akilinganisha mahali nchi ilipo kwa sasa, alisema Tanzania ina mafanikio katika miundombinu, kwa mifano ya maendeleo katika usafiri wa anga na reli, na kuhainisha mabadiliko makubwa katika huduma za kijamii kama elimu na afya.
Rais Samia mara baada ya kuwasili katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam zilipofanyika sherehe za miaka 60 ya Uhuru wa Tanganyika alipigiwa mizinga 21 ya heshima na kisha kuanza kukagua gwaride la majeshi mbalimbali.
Sherehe hizi zimehudhuriwa na Marais wa nchi mbalimbali wakiwemo Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta na Rais wa Rwanda, Paul Kagame, rais wa Comoro, Msumbiji na DRC.
Aidha, maadhimisho hayo yalipambwa na matukio mbalimbali yakiwemo burudani kutoka kwa watunzi watenzi, watoto wa halaiki, wasanii pamoja na vikosi mbalimbali vya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania JWTZ ambavyo vilipita Kikakamavu mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan.