Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema chanjo ya ugonjwa wa Corona ipo tayari nchini na ikiwa mwananchi yoyote anataka kuchanjwa akachanje kwa ajili ya kupata kinga dhidi ya ugonjwa huo.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo katika Baraza la Eid El Adha lililofanyika katika Msikiti wa Mtoro, Ilala jijini Dar es Salaam, Ambapo amesema ni vema kwa sasa wananchi wakajiepusha na mikusanyiko isiyokuwa ya lazima na wazingatie kukaa umbali wa mita moja au zaidi kutoka mtu mmoja hadi mwingine.
“Tumezipata hizo chache za aina kama mbili tatu, sisi tukasema basi tuzilete hapa nchini anayetaka achanje, kama unaona mwakani ni muhimu kwenda hijja basi fursa unayo hapa ndani. Lakini kama una ndugu zako, watoto wanasoma huko nje na nchi hiyo inataka waliochanjwa basi fursa iko ndani ya nchi usihangaike"- Waziri Mkuu Majaliwa.
Waziri Mkuu amesema ni vema kwa sasa wananchi wakajiepusha na mikusanyiko isiyokuwa ya lazima na wazingatie kukaa umbali wa mita moja au zaidi kutoka mtu mmoja hadi mwingine na pia wafanye mazoezi ya mara kwa mara kulingana na afya zao pamoja na mazingira yanayowazunguka, pamoja na kuzingatia kuzingatia lishe bora.
“Kwa wale wenye umri mkubwa na wenye uzito uliopitiliza na wenye magonjwa sugu kama moyo, pumu, kisukari na figo wanapaswa kuchukua hatua madhubuti zaidi kujikinga na ugonjwa huu.”-Majaliwa
Hata hivyo, Waziri Mkuu amewasisitiza wananchi wawahi katika vituo vya kutolea huduma za afya mara waonapo dalili za mafua makali, maumivu ya koo, kichwa kuuma, kupumua kwa shida, kukosa hamu ya kula na kupoteza uwezo wa kunusa harufu mbalimbali.”
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa rai kwa viongozi wa dini na waumini waendelee kuvumiliana, kustahamiliana na kushikamana katika kufanya ibada na kuienzi tunu ya amani.
“Tuendelee kufanya ibada, kuwaombea wenzetu waliotangulia mbele za haki, tuoneshane upendo na mshikamano hata baada ya kumalizika kwa masiku haya kumi bora ya Dhul Hijja.”-Aliongeza Waziri Mkuu.
Kwa upande wake, Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Sheikh Aboubakar Zubeir Bin Ally amewataka watanzania kuendelea kuimarisha maadili mema yatakayoisaidia taifa hili.
“Pia tumuombe Mwenyezi Mungu ili tuondokane na majanga yanayoikabili nchi yetu na ulimwengu mzima”-Mufti Mkuu.
Naye, Katibu Mkuu wa Baraza Kuu la Waislamu wa Tanzania (BAKWATA), Sheikh Nuhu Jabir Mruma amesema baraza hilo linatoa wito kwa waislamu na Watanzania kwa ujumla waendelee kuienzi na kuilinda amani wanaposherehekea sikukuu ya Eid Al-Adh’haa.
“Tunafanya hivi kwa kutambua kwamba amani ndio msingi wa maisha bora na yenye furaha kwa mwanadamu. Mwenyezi Mungu anatuelekeza juu ya faida ya amani katika kitabu chake kitukufu cha Qur’an sura ya 16 aya ya 112 na nanukuu “Na Mwenyezi Mungu amepiga mfano wa mji uliokuwa na amani na utulivu, riziki yake ikiufikia kwa nafasi kutoka kila mahali.”- Sheikh Jabir.
Waumini wa dini ya Kiisalamu wamesheherekea sikukuu ya Eid al Adha, Ambapo ni sherehe inayowataka kutekeleza suna ya kuchinja kama alivyofanya Nabii Ibrahimu.