Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali inathamini mchango wa Sekta Binafsi na Taasisi za Dini likiwemo kanisa Katoliki katika kuimarisha upatikanaji wa huduma mbalimbali za kijamii nchini.
Ametoa kauli hiyo leo Jumapili Julai 4, 2021 alipomuwakilisha Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan katika ibada ya kuwekwa wakafu na kusimikwa kwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Bunda, Askofu Simon Chibuga Masondole. Ibada hiyo imefanyika katika viwanja vya Kanisa Kuu Bunda, Mkoani Mara.
Amesema kuwa Serikali kwa upande wake itaendelea kushirikiana na madhehebu ya dini katika kutoa huduma hizo kwa Watanzania wote bila ubaguzi wa aina yoyote.
"Upo usemi usemao 'Kama unataka kwenda haraka tembea peke yako, lakini kama unataka kwenda mbali tembea na wenzako. Sisi wote tuna imani kubwa nawe kuwa utaendeleza mashirikiano mazuri yaliyopo baina ya Serikali na Kanisa"-Alibainisha Waziri Majaliwa.
Aidha, Waziri Mkuu amewataka Watanzania kutumia nyumba za ibada kuliombea Taifa ili waendelee kuishi kwa amani, upendo na mshikamano.
"Amani tuliyo nayo, ndiyo chachu kubwa ya kufikia mafanikio ya maendeleo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi"- Ameongeza Waziri Mkuu.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mara Ally Hapi amesema wataendelea kutoa ushirikiano usio na mashaka kwa askofu mteule na Kanisa Katoliki kwa kuwa wanatambua mchango wa Kanisa hilo katika mkoa wa Mara.
Jimbo la Bunda linapata Askofu wa pili tokea kuanzishwa miaka kumi iliyopita akichukua nafasi ya Askofu Renatus Nkwande ambaye ni Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Mwanza.