Mfanyabiashara maarufu ndani ya Tanzania na nje ya nchi Yusuf Manji anashikiliwa na mamlaka ya kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU akikabiliwa na tuhuma tatu, baada ya kurejea nchini akitokea nje ya nchi ambako alikaa muda mrefu.
Kwa mujibu wa Kamanda wa TAKUKURU kamishna wa Polisi Said Hamduni, amesema mfanyabiashara huyo anashikiliwa na taasisi hiyo tokea alipowasili nchini Tanzania akituhumiwa kukwepa kodi.
Kamishina Hamduni amesema kampuni zake za Intertrade Commercial LTD Service na Golden Globe International Service Limited zinatuhumiwa kwa kutolipa kodi ya VAT kati ya mwaka 2011 na 2015 wakati zikifanya biashara na Shirika la Umeme nchini Tanzania Tanesco Kupitia kampuni yake ya Golden Globe.
Tuhuma nyingine inayomkabili ni kupitia kampuni yake ya Quality Group kuhusu mapato ya klabu ya Yanga ambayo alikuwa akiidhamini na kuiongoza kama mwenyekiti wakati huo.
Manji amerejea nchini Tanzania siku chache baada ya Rais Samia Suluhu kuhimiza wafanyabiashara waliotoroka nchi kurejea na kuendelea na uwekezaji wao.