Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa siku tatu kwa Wizara ya Kilimo kukutana na menejimenti ya kampuni ya utengenezaji na usambazaji wa mbolea ya YARA ili kuhakiki na kupata ithibati ya mbolea ya bure.
Waziri Majaliwa ametoa kauli kwakuwa mbolea hiyo inapaswa kugawiwa bure kwa wakulima wadogo nchini kupitia mpango wa Action Africa.
Ametoa wito huo leo Oktoba 7, 2020 alipotembelea kiwanda cha YARA kilichoko jijini Dar es Salaam, Na ameipongeza kampuni ya YARA kwa uwekezaji mkubwa na utekelezaji wa mpango huo wenye thamani ya shilingi bilioni 16.5.
“Serikali inawashukuru sana YARA kwa kutoa mbolea kwa ajili ya wakulima nchini lakini ni muhimu ithibati ifanyike ili iruhusu mbolea iende kwa wakulima. Mpango huu ni mzuri kwa sababu unaendana na malengo ya Serikali katika kukuza sekta ya kilimo”-Waziri Majaliwa.
Waziri Mkuu amesema Serikali ina nia njema ya kuunga mkono wadau wanaosaidia sekta ya kilimo na amewahakikishia wawekezaji hao usalama na mazingira mazuri ya uwekezaji hapa nchini.
Pia, Waziri Mkuu ametoa wito kwa makampuni na taasisi nyingine kuiga mpango huo wa YARA.
Waziri Majaliwa amemuomba Balozi wa Norway nchini Tanzania, Bibi Elizabeth Jacobsen aanzishe Jukwaa la Biashara kwa Wafanyabiashara wa Tanzania na Norway ili wapata uzoefu wa kibiashara kutoka kila upande.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya YARA, Bw. Winston Odhiambo amesema mpango huo utawanufaisha wakulima wadogo 83,000 nchi nzima ambapo tani 12,500 za mbolea ya zitagawiwa bure kwa wakulima wa mahindi na mpunga.