Mwanamfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman ameshutumiwa kwa kutuma mamluki nchini Canada ili kumuua aliyekuwa afisa wa ujasusi wa Saudi.
Mpango huo wa mwanamfalme kumuua Saad al-Jabri ambao haukufanikiwa ulifuata muda mfupi baada ya mauaji ya mwanahabari aliyeuawa nchini Uturuki, Jamal Khashoggi, nyaraka zilizowasilishwa katika mahakama ya Marekani zimedai.
Bwana Jabri, afisa mstaafu wa serikali ya Saudi Arabia, alikimbilia ughaibuni miaka mitatu iliyopita, ambapo tangu wakati huo amekuwa akipewa ulinzi binafsi mjini Toronto.
Mpango huo wa mauaji inasemekana kuwa ulifeli baada ya maafisa wa mpaka wa Canada kuanza kushuku kikosi hicho walipokuwa wanajaribu kuingia nchini humo kupitia uwanja wa ndege wa kimataifa wa Toronto Pearson, nyaraka zilizowasilishwa mahakamani zinaonesha.
Kwa miaka mingi Bwana Jabri 61, alikuwa kiungo muhimu katika huduma ya ujasusi ya siri Uingereza na mashirika mengine ya kijasusi ya nchi za Magharibi nchini Saudi Arabia.
Malalamiko ya kurasa 106 ambayo bado hayajaidhinishwa, yalifunguliwa Washington DC, yakimshutumu mwanamfalme kwa kujaribu kumuua Bwana Jabri ili kumyamazisha.
Bwana Jabri anasema hilo ni kwasababu yeye anajua taarifa nyeti huku nyaraka hiyo inasema hayo ni pamoja na ufisadi na usimamizi wa kikundi cha mamluki nje ya nchi kilichopewa jina la kikosi cha Tiger.
Wanachama wa kikosi hicho cha mamluki cha Tiger walihusika na mauaji ya mwanahabari Khashoggi, aliyeuliwa ndani ya ubalozi wa Saudi, mjini Istanbul 2018, nyaraka iliyowasilishwa mahakamani inasema.
"Sehemu ya madai ni nyeti, ikiwa ni pamoja na tarifa za udhalilishaji na nyingine zenye ushahidi kuhusu mshtakiwa bin Salman na kumbukumbu ya Dkt. Saad inavyoangazia nukuu alizosema akibashiri kuuawa kwakwe," nyaraka hiyo inasema.
Aidha, baada ya kutoroka Saudi Arabia 2017, bwana Jabri alikimbilia Canada kupitia Uturuki.