Waandamanaji nchini Marekani wameingia mitaani katika majimbo kadhaa wakishinikiza magavana kufungua uchumi wa majimbo yao kwa kuondoa amri ya kutokutoka nje maarufu kama 'lockdown'.
Marufuku hiyo ya kutokutoka nje iliwekwa katika majimbo yote ya Marekani ili kudhibiti kusambaa kwa janga la virusi vya corona, hali iliyotikisa uchumi wa taifa hilo kubwa zaidi kiuchumi duniani.
Majimbo yaliyoripotiwa kuwa na maandamano jana Jumapili ni Arizona, Colorado, Montana na Washington, huku mwendelezo wa maandamano hayo ukitarajiwa leo Jumatatu.
Hasira juu ya marufuku hizo imeongezeka nchini humo huku waandamanaji wakitaka masharti yalegezwe licha ya hatari ambayo ingalipo ya maambukizi ya virusi vya corona.
Kwa sasa, Marekani ndiyo kitovu cha janga la ugonjwa wa virusi vya corona (COVID-19), kukiwa na wagonjwa zaidi ya 735,000 na vifo zaidi ya 40,000.
Hata hivyo kuna dalili kuwa maambukizi yanafikia kileleni nchini humo na kasi ya maambukizi kuanza kushuka katika baadhi ya majimbo.
Magavana katika majimbo mbalimbali wameanza majadiliano ya kufungua uchumi baada ya kushuhudiwa kupungua kwa maambukizi, lakini maeneo mengine bado yangali kwenye marufuku kali, Gavana wa New York Andrew Cuomo ametangaza kuongeza muda wa marufuku wiki hii katika jimbo lake mpaka kufikia Mei 15.