Rais Donald Trump wa Marekani amethibitisha kwamba jeshi la Marekani limemuua kiongozi wa al Qaeda katika rasi ya Uarabuni Qassem al-Rimi, katika operesheni yake ya kukabiliana na ugaidi nchini Yemen.
Al-Raymi anatajwa kuwa ni mwanzilishi wa al Qaeda katika rasi ya Uarabuni na kundi hilo analoliongoza ndilo lililodai kuhusuika na shambulizi la Jumapili iliyopita katika kambi ya kijeshi ya Wamarekani ya kikosi cha wanamaji na kuwauwa wanajeshi watatu.
Taarifa kutoka ikulu ya Marekani zinasema kuwa Qasim al-Raymi ambaye aliongoza kikundi cha Jihad tangu mwaka 2015, aliuawa wakati wa operesheni ya majeshi ya Marekani nchini Yemen.
Kiongozi huyo wa wapiganaji wa Jihad amekuwa akihusishwa na mfululizo wa mashambulizi dhidi ya maslahi ya nchi za Magharibi katika miaka ya 2000.
Alichukua madaraka ya uongozi baada ya mtangulizi wake kuuawa kwa shambulio la ndege zisizo na rubani za Marekani.
Kundi hilo la AQAP liliundwa mwaka 2009 kutokana na matawi mawili ya Al-Qaeda nchini Yemeni na Saudi Arabia, ikiwa na nia ya kuangusha tawala za serikali zinazoungwa mkono na Marekani na kuondoa ushawishi wa nchi za Magharibi kwenye ukanda huo.
Tetesi kuhusu kifo cha al- Raymi kwa shambulizi la Marekani zilianza kusambaa mwishoni mwa mwezi Januari. Katika kujibu hilo kundi hilo lilitoa ujumbe wa sauti ukiwa na sauti ya al -Raymi tarehe 2 mwezi Februari ukisema kuwa wao ndio waliotekeleza shambulio la risasi kwenye kambi ya jeshi la wanamaji wa Marekani huko Pensacola, Florida.
Taarifa kutoka Ikulu ya Marekani sasa imethibitisha kifo cha Al-Raymi lakini bado haijasema aliuawa lini.
Mwisho.