Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ameahidi kulijenga upya kanisa kuu Katoliki la Notre Dame mjini Paris ambalo liliungua moto jana jioni na kusababisha uharibifu katika sehemu ya jengo hilo. Kanisa la Notre Dame lilijengwa karne ya 12 na limekuwa ni mojawapo ya vivutio vya utalii nchini Ufaransa. Kanisa hilo lilikuwa chini ya ukarabati ambao umetajwa na vyombo vya habari vya ndani kuwa chanzo cha moto. Moto huo umeunguza na kuangusha mnara wa juu wa kanisa ulio na urefu wa mita 93 ambao umekuwa ni alama ya utambulisho, lakini mkuu wa kikosi cha Zimamoto Jean-Claude Gallet amesema sehemu kubwa ya Kanisa imeweza kuokolewa baada ya maafisa kuzuia moto kuenea zaidi. Viongozi mbalimbali ulimwenguni wametuma salamu za pole kutokana na mkasa huo ambapo Kansela Angela Merkel amelielezea kanisa hilo kuwa ishara ya Ufaransa na utamaduni wa Ulaya.
CHANZO: Idhaa ya kiswahili ya DW