Wapiganaji wa Taliban wamepiga marufuku na kutoa maagizo kwa vinyozi katika mkoa wa Helmand nchini Afghanistan kutowanyoa au kuwapunguza ndevu wanaume, wakisema hatua hiyo inakiuka sheria ya Kiislamu.
Maagizo hayo yanasema kuhusu kurudishwa kwa sheria kali kama zile zilizokuwepo wakati kundi hilo lilipokuwa madarakani awali , licha ya ahadi ya kwamba litaanzisha serikali itakayokuwa na misimamo ya wastani.
"Mtu yoyote anayekiuka sheria hiyo ataadhibiwa’’, Askari wa Taliban wamesema.
Baadhi ya vinyozi katika mji wa Kabul wamesema kwamba pia wao walipata maagizo kama hayo.
Tangu ilipochukua madaraka mwezi uliopita, Talibani imewapatia adhabu kali wapinzani wake.
Siku ya Jumamosi, wapiganaji wa kundi hilo, waliwapiga risasi na kuwaua watekaji wanne na miili yao kuzungunshwa katika barabara ya mkoa wa Herat.
Katika ilani iliochapishwa katika saluni, kusini mwa mkoa wa Helmand , maafisa wa Taliban walionya kwamba vinyozi lazima wafuate sheria ya Kiislamu katika kunyoa nywele za kichwani na ndevu.
Hakuna hata mtu mmoja aliye na uwezo wa kulalamika, ilisema notisi ilioonekana na BBC.
"Wapiganaji hao wanaendelea kuja na kutuagiza kutonyoa ndevu’’, alisema kinyozi mmoja mjini Kabul.
Aidha, Wakati wa uongozi wa kwanza wa Taliban kuanzia 1996 hadi 2001, Kundi hilo lilipiga marufuku mitindo tofauti ya nywele na kusisitiza kwamba wanaume wafuge ndevu.
Lakini tangu wakati huo, unyoaji wa ndevu na nywele fupi miongoni mwa wanaume wa Afghan umekuwa maarufu.
#ChanzoBBCSwahili