Baraza la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa limeanza kikao maalum leo kuhusu Israel ambapo Mkuu wa haki za bindamu wa Umoja huo Michelle Bachelet amesema mashambulizi mabaya ya Israel dhidi ya Gaza huenda yakawa yamesababisha uhalifu wa kivita ikiwa yatabainika yalipindukia mipaka.
Kikao hicho kimeitishwa kutokana na ombi la nchi za kiislamu.Kikao hicho kinafanyika baada ya waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken kumaliza ziara yake mashariki ya kati na leo alhamisi ameelekea nyumbani Marekani.Kituo chake cha mwisho kilikuwa Jordan ambako alitowa mwito wa ushirikiano wa kikanda kuimarisha makubaliano ya kusitisha vita baina ya Israel na wanamgambo wa Gaza. Kadhalika waziri huyo wa mambo ya nje wa Marekani jana alikutana na rais wa Misri AbdelFatah al Sisi mjini Cairo ambapo alimpongeza kwa kusaidia kumaliza vita vikali. Wizara ya afya mjini Gaza imesema mashambulizi ya anga ya wanajeshi wa Israel yaliyofanywa dhidi ya Gaza yaliwauwa wapalestina 254 wakiwemo watoto 66 na watu 1,900 walijeruhiwa kufuatia siku 11 za vita.
CHANZO: IDHAA YA KISWAHILI (DW)