Mkosoaji wa utawala wa Kremlin nchini Urusi Alexei Navalny ameandika katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa instagram kwamba anazuiliwa katika kambi ya mateso eneo la Vladimir Kaskazini Mashariki mwa mji mkuu, Moscow.
Katika taarifa hiyo Navalny amesema anazuiliwa katika eneo lenye ulinzi mkali la gereza hilo.
Navalny alikuwa hajulikani aliko baada ya timu yake ya mawakili kusema wiki iliyopita kwamba alikuwa amehamishwa kutoka gereza la Kolchugino na kwamba hawakujulishwa alikopelekwa.
Vyombo vya habari vya Urusi vimemnukuu wakili wa Navalny Olga Mikhailova akithibitisha anazuiliwa katika gereza hilo akisema hajafanikiwa kwenda kumtembelea.
Navalny mwenye umri wa miaka 44 alipelekwa gerezani mapema mwaka huu kwa kukiuka masharti ya msamaha wake, uamuzi ambao nchi za Magharibi zimeukosoa zikisema ulichochewa kisiasa.