Rais Donald Trump amelihutubia taifa la Marekani kabla hajaondoka madarakani na kusema kuwa; "Tumefanya kile ambacho tulikuja kukifanya na tumefanya mambo mengine mengi."
Katika video aliyoiweka kwenye mtandao wa YouTube, alisema "mapambano yalikuwa makali, vita ilikuwa ngumu kwasababu hicho ndicho mlinichagua kukifanya".
Bwana Trump anaondoka madarakani akiwa bado hakubaliani na matokeo ya uchaguzi wa Novemba 2020, ambao ulimuibua Joe Biden kuwa rais.
Wiki mbili za mwisho za utawala wa bwana Trump',umekumbwa na ghasia baada ya wafuasi wake kuvamia jengo la bunge la Capitol Hill, wakipinga matokeo ya uchaguzi.
"Ghasia za kisiasa ni shambulio la kila kitu tunachothamini kama Wamarekani. Kamwe hatuwezi kuvumilia," Bwana Trump alisema katika video yake, ambapo bado hakutambua ushindi wa mrithi wake.
Bwana Trump mwenyewe ameshtakiwa kwa uchochezi juu ya shambulio la uvamizi wa bunge na atakabilina na kesi hiyo baada ya kuondoka madarakani. Ikiwa atakutwa na hatia, anaweza kuzuiwa kufanya shughuli zozote za umma.
Trump ni rais wa kwanza kushtakiwa mara mbili. Kesi yake ya kwanza ilimuhusisha na kutumia wadhifa wake vibaya nchini Ukraine lakini alifanikiwa kushinda kesi hiyo baada ya kupata kura nyingi kutoka kwa chama chake cha Republican.
Katika ujumbe wake, Trump alisema utawala wake umeweza kujenga uchumi wa Marekani kwa kiwango cha juu zaidi katika historia ya dunia.
Soko la hisa la Marekani limeongezeka, ingawa uchumi bado uko katika wakati mgumu kutokana na janga la corona.
Chanzo na BBC Swahili.