Hatua iliyotangazwa wiki iliyopita na Ethiopia ya kuanza kwa zoezi la kujaza bwawa kubwa la kuzalisha umeme la Renaissance kwenye Mto Nile linaendelea kuzua mvutano na nchi jirani zilizo na mto huo.
Kazi katika mradi wa bwawa la maji la kuzalisha umeme huko Ethiopia imeshika kasi, huku jaribio la kuutatua mgogoro wa Ethiopia na nchi jirani zinazopakana na mto Nile zikiendelea.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres Jumanne wiki hii aliziataka Ethiopia, Sudani na Misri kuwa na "uvumilivu" katika juhudi zao za kufikia makubaliano, ambapo mazungumzo ya Washington yalisitishwa tangu mwezi Februari.
Katikati ya mzozo huo ni mpango wa kujaza bwawa hilo kuu, Ethiopia inataka kutekeleza mpango huo kwa kipindi cha miaka sita, Misri ikipendekeza muda wa miaka kumi ikihofu mradi huo utafanya Ethiopia kudhibiti maji ya mto Nile.
Mradi huu unaotarajiwa kuanza kuzalisha umeme kuanzia mwaka 2022 utagharimu dola bilioni nne za kimarekani, Ni mradi mkubwa lakini umesababisha pia mgogoro wa kidiplomasia kati ya Misri na Sudan kwani nao wanategemea maji ya mto Nile.
Bwawa hilo linalojengwa Kaskazini mwa Ethiopia, litakuwa kituo kikubwa kabisa cha kuzalisha umeme barani Afrika.
Lakini Misri, ambayo inategemea maji ya mto Nile kwa 80%, ina hofu kuwa bwawa hilo litaathiri mfumo wa usambazaji maji ambao nao una changamoto kadhaa.
Mara baada ya kukamilika, bwawa hilo litakalokuwa na uwezo wa megawatt 6000 litakalogharimu pauni bilioni tatu, lakini ujenzi huo umeathiriwa na ucheleweshaji na haijafahamika kama litaanza kufanya kazi baada ya muda wa mwisho uliowekwa na serikali mwaka 2021.
Bwawa hilo lenye urefu wa mita 145, karibu kilometa 2 linatarajiwa kuwa chanzo kikubwa cha kuzalisha umeme nchini Ethiopia.