Kiongozi wa zamani wa kundi la waasi katika Nchi ya jamhuri ya kidemokrasi ya Congo Germain Katanga aliyekuwa amehukumiwa kifungo cha miaka 12 katika mahakama ya kimataifa ICC, amechiliwa huru.
Hatua hii ya kumwachilia huru Germain Katanga imekuja siku moja baada ya kuachiwa huru kwa kiongozi mwengine wa waasi wa UPC Thomas Lubanga jijini Kinshasa nchini humo.
Shirika la habari la rfi Swahili limeripoti kuwa taarifa ya kuachiwa kwake huru imetolewa hapo jana na mpwa wake Jeannot Malivo Kagaba huko Kinshasa na kuthibitishwa na mkuu wa shirika lisilokuwa la kiserikali linalotetea haki za wafungwa Emmanuel Cole, na ambaye aliiambia AFP kuwa ni baada ya kukamilishwa kwa hatua zote za kisheria.
Katanga mwenye umri wa miaka 43, alihukumiwa kifungo cha miaka 12 Mwaka 2014 kwa kosa la uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya ubinadamu katika shambulio la kijiji huko Ituri pia alihusika katika mauaji ya watu takribani 200 mnamo mwaka 2003 Kaskazini mashariki mwa DRC.
Mwisho.