Kulingana na matokeo rasmi ya awali yaliyotangazwa usiku wa Jumapili kuamkia leo Jumatatu na Tume huru ya taifa ya uchaguzi, Faure Essozimna Gnassingbé amechaguliwa tena kwenye muhula wa nne kama rais wa Togo.
Bwana Faure ambaye alikuwa mgombea kupitia chama cha UNIR, ametangazwa kuwa rais wa Jamhuri ya Togo na hii ni kulingana na Tume ya Uchaguzi nchini humo CENI kutangaza matokeo, ambapo Faure amechaguliwa tena katika duru ya kwanza ya uchaguzi wa urais kwa asilimia 72.36 ya kura.
Upande wa upinzani, Waziri Mkuu wa zamani na mpinzani mkuu wa Bw Gnassingbé, Agbéyomé Kodjo amepata asilimia 18.37 ya kura.
Huku kiongozi wa ANC, Jean-Pierre Fabre ameshika nafasi ya tatu kwa asilimia 4.35.
Ni mara ya kwanza Tume huru ya kitaifa ya uchaguzi kutangaza haraka matokeo ya uchaguzi wa urais nchini humo licha ya kwamba matokeo hayo yatapelekwa kwenye Mahakama ya Katiba, ambayo ina siku sita ya kuchunguza na kutangaza matokeo ya mwisho.
Kupitia akaunti yake ya Twitter, Faure amewashukuru vijana wa Togo ambao amewataka kusherehekea ushindi huo walioupata kupitia chama chale cha UNIR.
Aidha, matokeo hayo yaliyompa ushindi Faure tayari yamepingwa huku mashirika ya kiraia yamegundua visanduku vya kura ambavyo vilijazwa kura kabla ya uchaguzi na kubaini kwamba matokeo ya uchaguzi yamebadilishwa.
Tangu Jumamosi jioni, na hata kabla ya kutangazwa kwa matokeo na tume ya uchaguzi ya nchini Togo CENI, Agbéyomé Kodjo ameshutumu kuwepo kwa "udanganyifu mkubwa" katika uchaguzi huo.
Kodjo alifanya mkutano na waandishi wa habari jijini Lomé, akithibitisha kwamba kulingana na takwimu alizo nazo, bila shaka yeye ndio mshindi wa uchaguzi na kumtaka Faure kukubali kushindwa.
Mwisho.