Polisi wa Kiislamu katika jimbo la Kano inayofahamika kama Hisbah imemkamata mwanaume mwenye umri wa miaka 26 kwa jina Aliyu Na Idris ambaye taarifa yake imekuwa ikienea kwenye mitandao ya habari ya kijamii wikiendi iliyopita kwa kutangaza kuwa anataka anunuliwe kutokana na "umasikini".
Kamanda wa Hisbah Harun Ibn Sina ameithibitishia BBC kukamatwa kwake, na kuongeza kuwa vitendo vya Aliyu Na Idris vimezuiwa.
"Ndio tulimkamata Jumanne na amekuwa pamoja nasi usiku, kile alichokifanya kinazuiwa katika Uislamu, huwezi kujaribu kujiuza hata uwe katika hali gani."
Fundi huyo wa nguo aliyekamatwa, alikuwa akizungumza na waandishi wa habari nchini Nigeria, akisema kwamba alikuwa na matatizo makubwa ya kifedha, ndio maana akaamua kujiuza kwa Naira Milioni 20 ($49,000; £35,000) ambayo ni bei aliyokuwa ameichapisha kwenye bango alilotembea nalo kwa mtu yeyote ambaye angempatia maisha yake yote.
"Nitawapa wazazi wangu Naira Milioni 10 ($24,000; £18,000)".
Pia nitalipa naira milioni tano kama kodi ya jimbo kama wataninunua ($12,000; £9,000), nitampatia Naira Milioni 2 ($5,000; £4,000) mtu aliyenisaidia kutangaza kuuzwa kwangu, na pesa zitakazobaki nitazitumia kufanya biashara kwa ajili ya kujikimu katika maisha yangu ya kila siku."