Kiongozi wa upinzani nchini Zambia Hakainde Hichilema ameibuka mshindi wa uchaguzi mkuu wa Urais.
Alikuwa akikabiliana na mpinzani wake wa siku nyingi kutoka chama tawala Edgar Lungu ambaye alidai kwamba uchaguzi huo haukuwa huru na wa haki baada ya kupoteza kura nyingi katika ngome zake.
Lakini kikijibu madai hayo chama cha bwana Hichilema cha United Party for National Development kilisema kwamba taarifa hiyo ni hatua za mwisho za utawala unaondoka.
Baada ya kujumlisha kura zote tume ya uchaguzi ilisema kwamba bwana Hichilema alishinda kwa kujipatia kura 2,810,777 huku Lungu akijipatia 1, 814, 201 katika uchaguzi huo wa siku ya Alhamisi.
"Natangaza kwamba Hichilema ndiye rais wa Zambia"-Alisema mwenyekiti wa tume hiyo Esau Chulukatika kituo cha kutoa matokeo kilichopo mjini Lusaka.
Uongozi wa miaka sita wa bwana Lungu ulikosolewa kwa madai ya kukiuka haki za binadamu, ufisadi na uchumi uliodorora pamoja na ukosefu wa ajira.
Lungu alisema kwamba maafisa wa chama chake cha Patriotic Front walifukuzwa kutoka katika vituo vya kupigia kura, wakiacha kura bila ulinzi wowote.
Ushindi huo mkubwa unaamanisha kwamba bwana Hichilema hatoshiriki katika awamu ya pili ya uchaguzi, Ambapo kulikuwa na jumla ya wapiga kura milioni saba waliojisajili kushiriki katika uchaguzi huo.