Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Felix Tshisekedi, katika hotuba yake kwa taifa aliyoitoa siku ya Ijumaa wiki hii ametangaza nia yake ya kufungua mashauriano na viongozi wa vyama vya kisiasa kuanzia wiki ijayo.
Katika hotuba yake iliyodumu takribani dakika 6, Rais Tshisekedi amemuonya mshiriki wake katika muungano tawala, FCC ya mtangulizi wake Joseph Kabila.
Baadhi walitarajia kuvunjika kwa muungano tawala unaoundwa na miungano ya vyama ya CACH na FCC, wengine walitarajia kuteuliwa kwa waziri mkuu kwa minajili ya kuunda serikali mpya.
Mvutano kati ya FCC na CACH bado unaendelea siku chache baada ya kuapishwa majaji wa tatu wa walioteuliwa hivi karibuni na rais Félix Tshisekedi.
Duru kutoka ikulu ya rais Tshisekedi zinaeleza kwamba rais alikasirishwa na uamuzi wa Waziri Mkuu Sylvestre Ilunga na mawaziri wake kutohudhuria hafla ya kuapishwa kwa majaji watatu miongoni mwa tisa walioteuliwa na rais mwezi Julai.
FCC na CACH wanatofautiana katika mambo mengi, Ambapo miongoni mwa tofauti hizo kuna mageuzi katika tume ya uchaguzi, haswa muundo wa Tume ya Uchaguzi, lakini Félix Tshisekedi pia anataja amani na usalama wa kitaifa, diplomasia au kuanzishwa kwa taifa lenye sheria mageuzi ambayo yanawakera baadhi ya wapinzani wake kutoka muungano wa FCC.
Katika kile kinachoashiria kuwa ni mvutano wa wazi baina ya rais Tshisekedi na mtangulizi wake Joseph Kabila, muungano wa FCC ulitangaza jana kwamba uko tayari kusitisha muungano wake na chama cha UDPS cha rais Tshisekedi.