Waziri wa Usafirishaji wa Kenya James Macharia amesema wanatarajia kutuma ndege ya Kenya Airways nchini China siku ya Jumatano kwa ajili ya kuchukua vifaa vya kupambana na ambavyo vitatumika kuzuia kuenea kwa maambukizi ya Corona ugonjwa.
Waziri Macharia ametoa taarifa hiyo wakati akitangaza kuongezwa muda wa marufuku ya ndege za kigeni kuingia nchini Kenya kwa muda wa siku 30 nyingine, na kuruhusu ndege za mizigo tu na zile za kuhamisha raia wa kigeni ambazo zitaendelea kufanya kazi.
Aidha, nchi ya Kenya imethibitisha kuwa na wagonjwa wapya 16 wa corona, baada ya kuwafanyia vipimo watu 530, na mpaka sasa Kenya imefikisha idadi ya watu 142 wenye maambukizi ya COVID-19.
Wizara ya Afya ya Kenya imetangaza kuwa katika kesi hizo mpya 16 za maambukizi ya corona nchini humo, raia wa Kenya ni 15 na mmoja ni raia wa Nigeria, raia 11 kati ya hao wana historia ya kusafiri nje ya nchi na watano kati yao wameambukizwa wakiwa ndani ya Kenya, watu 12 ni kutoka mji mkuu wa Kenya Nairobi, wengine watatu wanaishi Mombasa na mmoja ni kutoka Kilifi.
Waliokutwa na maambukizi mapya wana umri kati ya miaka 22 na 66, wanaume ni tisa na wanawake saba.
Vilevile Wizara ya Afya ya Kenya imesema kuwa inatengeneza barakoa (maski) ambazo zitasambazwa kwa wananchi hivi karibuni, na pia imesema watu watakaokufa kwa corona watazikwa ndani ya masaa 24 huku watu wa karibu wa familia wasiozidi 15 ndio wataruhusiwa kuhudhuria mazishi hayo yatakayosimamiwa na Serikali.
Mwisho.