Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa ametangaza ongezeko la visa viwili vya wagonjwa wenye maambukizi ya virusi vya corona.
Watu hao waliogundulika na virusi vya ugonjwa huo ni raia wawili wakigeni, mmoja amepatikana akiwa Zanzibar ambaye ni raia wa Ujerumani na mwingine yupo Dar es Salaam ambaye ni raia kutoka nchini Marekani.
Waziri wa afya Ummy Mwalimu siku ya Jumatatu Machi 16, 2020 alitangaza kuwepo kwa kisa cha kwanza cha mtu mwenye maambukizi ya mgonjwa mmoja mwenye maambukizi ya virusi vya Corona ambaye ni mwanamke na alikuwa ni Mtanzania.
Mpaka kufikia siku ya Jumanne Machi 17, 2020 Waziri Mkuu Majaliwa alitangaza kufunga shule zote (za awali, msingi na sekondari) kwa siku 30 na leo asubuhi Machi 18, 2020 Waziri Mkuu ametangaza vyuo vikuu vya elimu ya kati na vyuo vikuu kusitisha masomo ikiwa ni hatua ya kuzuia kuenea kwa maambukizi ya corona nchini humo.
Ameitaka wizara ya elimu kuafanya marekebisho ya ratiba ya mitihani ya kidato cha sita ambao walitarajiwa kufanya mitihani tarehe 4 Mei, itasogezwa mbele kadiri ya matokeo yatakavyojitokeza ili nao wapate kusoma kwa kipindi kilekile kilichokubalika na ratiba hiyo.
Michezo yote inayokusanya makundi ya watu kama vile ligi kuu ya Tanzania, Ligi daraja la pili, ligi daraja la kwanza lakini pia michezo ya shule za msingi (UMITASHUMTA) , michezo ya shule za sekondari(UMISETA) pamoja na michezo ya mashirika ya umma imetangazwa kusitishwa na Waziri Mkuu kuanzia jana.
Waziri Mkuu Majaliwa amesma kuwa nchi imejiandaa vyema kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa wa huu wa Corona.
Mwisho.