Uchaguzi wa Bunge nchini Ethiopia ambao awali ulikuwa umepangwa kufanyika baina ya mwezi Mei na Juni, sasa utafanyika mwezi Agosti mwaka huu.
Hayo yameelezwa na Bi Birtukan Mideska, Mkuu wa Tume ya Uchaguzi ya Ethiopia ambaye ametangaza kuwa, tume yao imependekeza tarehe 16 mwezi Agosti iwe ndio siku ya kufanyika uchaguzi huo wa Bunge.
Mkuu huyo wa Tume ya Uchaguzi ya Ethiopia ametoa tangazo hilo katika mkutano wake na vyama vya siasa pamoja na asasi za kijamii.
Kwa mujibu wa Tume ya Uchaguzi ya Ethiopia, uamuzi wa kusogeza mbele zoezi la uchaguzi wa Bunge umechukuliwa kutokana na kutokamilika kwa maandalizi ya uchaguzi huo ambapo si vyama vya siasa wala waandalizi wa uchaguzi huo ambao wako tayari kufanya zoezi hilo mwezi Mei.
Uchaguzi huo wa Bunge unatarajiwa kuwa wa kwanza chini ya uongozi wa Waziri Mkuu Abiy Ahmed ambapo mshindi huyo wa tuzo ya Nobel alichukua wadhifa wa Waziri Mkuu wa Ethiopia Aprili mwaka 2018 na kufanikiwa kufanya mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kisiasa.
Awali vyama vya upinzani nchini Ethiopia vimetahadharisha kuhusiana na hatua yoyote ile inayolenga kuahirisha uchaguzi huo wa Bunge, kama ambavyo tayari baadhi ya vyama vya siasa vimelalamikia uamuzi huo mpya wa Tume ya Uchaguzi.
Hivi karibuni Waziri Mkuu wa Ethiopia alinukuliwa akisema kuwa, kuwa nchi yake inakabiliwa na changamoto nyingi katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi wa Bunge, ambapo suala la usalama na vifaa vya kuendeshea zoezi hilo ni miongoni mwa changamoto hizo.
Mwisho.