Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Pombe Magufuli ametekeleza ahadi ya kulipa fidia ya zaidi ya shilingi bilioni 3 kwa wakazi ambao wanapisha ujenzi wa daraja la Kigongo Busisi jijini Mwanza.
Itakumbukwa disemba 7 mwaka 2019, Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Jphn Pombe Magufuli aliagiza kulipwa fidia kwa wakazi watakaopisha mradi wa ujenzi wa daraja la Kigongo Busisi na wakazi ambapo alisema wakazi hao wanapaswa kulipwa fiidia zao mapema ili kuepusha usumbufu.
Hatua hiyo ya kutimiza adhma hiyo ya kuwalipa fiidia watu 165 na makaburi 78 kwa mujibu wa uthamini uliopitishwa maeneo ya Kigongo na Busisi,ni zoezi linalosimamiwa na wakala wa barabara Tanzania TANROAD Mkoa wa Mwanza.
Mhandisi Pius Mwami ambaye ni Kaimu Meneja wa TANROAD mkoa wa Mwanza amesema tayari fedha zimeshafika na utaratibu wa kuzilipa kwa wananchi umeshaanza.
“Napenda kuwataarifu wananchi kuwa agizo la Mhe.Rais alilolitoa disemba 09,2019 tayari amelitekeleza na pesa zimeletwa ambazo ni shilingi bilioni 3.145 kwa ajili yakulipa nyumba, viwanja, na makaburi ambapo barabara inapita kwenda kuunganisha daraja litakapojengwa”; Mhandisi Pius Mwami - Kaimu Meneja wa TANROAD Mwanza
Mmoja wa wananchi aitwaye Lucas Sylvester ambaye ni miongoni mwa wananchi waliopokea hundi za malipo amekuwa radhi kwa kile alichokipata;
“Naipongeza serikali kwa hatua inazochukua kwababu hii sisi wananchi tumekubali kupisha maendeleo kwasababu maendeleo tunayaona”;Lucas Sylvester-Mkazi wa Kigongo.
Mtendaji wa Kijiji cha Kigongo Bi. Plased Valentine amesema serikali imejidhatiti kuwalipa fidia wananchi wote watakaokuwa wanapisha miradi ya maendeleo kulingana na taratibu na kanuni zilizopo nchini na amewataka wananchi watakaohama kujenga makazi upya na hata kuwasihi kwa kutoa angalizo la nidhamu ya fedha hizo.
“Fedha walizozipata wasiende kuzitumia vibaya, waende kuzitumia katika malengo waliyoyapa kipaumbele kuyatekeleza hususani kujenga na tayari tumezungumza nao matumizi sahihi ya hizi fedha.”;Plased Valentine - Mtendaji Kijiji cha Kigongo
Aidha, baada ya malipo hayo wananchi wamepewa mwezi mmoja kuondoka ndani ya eneo hilo ili kupisha ujenzi wa mradi wa daraja hilo na zoezi la ulipaji wa fidia hizo linafanyika kwa awamu ambapo mpaka sasa watu 33 kutoka eneo la busisi wilaya ya Sengerema tayari wamelipwa.
Mwisho.