Waziri wa ulinzi wa Ufaransa amesitisha mazungumzo na mwenzake wa Uingereza huku pakiwa na mzozo uliochochewa na makubaliano mapya ya usalama kati ya Uingereza, Marekani na Australia.
Paris imekasirika baada ya Australia kutia saini makubaliano ya Aukus ya kujenga nyambizi zinazotumiaa nyuklia, ikiondoa mkataba mkubwa na Ufaransa katika mchakato huo.
Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson alisema Ufaransa haikuwa na wasiwasi wowote juu ya mpango huo.
Lakini mkutano wa Florence Parly na Katibu wa Ulinzi wa Uingereza Ben Wallace huko London wiki hii umefutwa.
Lord Ricketts, balozi wa zamani wa Uingereza nchini Ufaransa ambaye alifaa kuwa mwenyekiti mwenza wa siku mbili za mazungumzo, alithibitisha mkutano huo "umeahirishwa hadi tarehe nyingine".
Makubaliano ya Aukus yaliyoafikiwa wiki iliyopita, yanayoonekana kama juhudi ya kukabiliana na ushawishi wa China katika Bahari ya Kusini mwa China inayoshindaniwa, yalimaliza makubaliano yenye thamani ya $ 37bn (£ 27bn) yaliyosainiwa na Australia mnamo 2016 kwa Ufaransa kujenga manowari 12 za kawaida.
Waziri wa mambo ya nje wa Ufaransa Jean-Yves Le Drian ameielezea kama "kuchomwa kisu mgongoni" jambo ambalo alitaja kuwa "tabia isiyokubalika kati ya marafiki na washirika".