Rais wa Iran Hasan Rouhani amesema mauaji ya mwanasayansi wake wa masuala ya nyuklia hayatalemaza mpango wa nyuklia wa nchi hiyo.
Ameilaumu Israel kwa kuhusika na mauaji ya Mohsen Fakhrizadeh nje ya mji mkuu wa Tehran, siku ya Ijumaa - akisema ilionesha wazi kiwango cha chuki na kubabaika kwa maadui wake.
Israel haijatoa tamko lolote kuhusiana na madai hayo, lakini iliwahi kumshtumu mwanasayansi huyo kwa kuhusika na mpango wa kisiri wa kuunda silaha za nyuklia.
"Kwa mara nyigine tena, mikono ya maadui wa ulimwengu waliojawa na kiburi wametuulia mtu wetu," (maneno ya Rais Rouhan aliyotumia kuashiria Israel), alisema katika taarifa, kwa mujibu wa televisheni ya kitaifa.
Fakhrizadeh alifariki hospitali baada ya kushambuliwa mjini Absard, katika kaunti ya Damavand.
Hossein Dehghan, mshauri wa kijeshi wa kiongozi mkuu wa kidini wa Iran Ayatollah Ali Khamenei, ameapa "kuwashambulia" watu waliotekeleza mauaji hayo kama radi.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Mohammad Javad Zarif, amelaani mauaji hayo na kusema kuwa ni "kitendo cha ugaidi wa kitaifa -an act of state terror".
Mashirika ya ujasusi ya magharibi yanaamini Fakhrizadeh alikuwa anasimasimamia mpango wa kisiri wa uundaji silaha za nyuklia za Iran.
Madini ya urani ni kiungo muhimu katika utengenezaji wa kawi ya nyuklia na silaha za kijeshi za nyuklia.
Mohsen Fakhrizadeh, alikuwa mkuu wa kitengo cha utafiti na uvumbuzi katika wizara ya ulinzi, Jina la Fakhrizadeh lilitajwa na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu katika maelezo yake kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran mwezi April mwaka 2018.
Israel haijatoa tamko lolote kuhusiana na taarifa za mauaji ya mwanasayansi huyo.Pentagon pia imekataa kutoa kutoa kauli yoyote, kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters.