Umoja wa Falme za Kiarabu, (UAE) umesitisha utoaji viza kwa Wakenya na mataifa mengine 12 ya Kiislamu
Chanzo cha ndani kilichozingumza na shirika la habari la Reuters kimesema chanzo cha kusitishwa kwa utoaji visa ni sababu za kiusalama lakini hakuna taarifa zozote za kina zilizotolewa.
Kulingana na nyaraka iliotolewa, nchi nyingi zilizoathirika ni za Kiislamu yaani Iran, Syria, Afghanistan na Pakistan.
Nyaraka hiyo iliotumwa kwa makampuni yanayoendesha shughuli za visa iliyoonesha kwamba inaanza kutekelezwa Novemba 18.
Aidha, nyaraka hiyo pia ilionesha marufuku ya kutolewa kwa visa mpya za ajira pamoja na za raia wa kigeni nje ya UAE, wanaotaka kutembelea nchi hiyo wa nchi 13 pamoja na Somalia, Libya na Yemen hadi siku isiyojulikana.
Serikali ya Kenya bado haijatoa tamko lolote kuhusiana na hatua hiyo sawa na mamlaka husika ya UAE ambayo baada ya kuzungumza na Shirika la Habari la Reuters haikusema lolote.
Hatua hiyo inawadia wiki moja baada ya Ubalozi wa Ufaransa nchini UAE kusihi raia wake kuchukua tahadhari baada ya kutokea kwa shambulizi la bomu dhidi ya wanadiplomasia nchini Saudi Arabia huku wanamgambo wa Islamic State wakadai kuhusika.
Itakumbukwa kuwa mwaka 2019 uhusiano kati ya Kenya na UAE uliathirika kufuatia kashfa iliyozunguka biashara ya dhahabu iliyokuwa ikielekea katika taifa hilo la Kiarabu
Mtawala wa Dubai Sheikh Mohammed Al-Makhtoum, alituma barua ya pingamizi kwa Kenya akitaka kuachiliwa kwa mzigo wa dhahabu uliokuwa ukizuiliwa na idara ya forodha mjini Nairobi.
Kesi hiyo ndio ya hivi karibuni inayowahusisha washirika wa Sheikh al-Makhtoum ambao wamehujumiwa katika biashara ya dhahabu nchini Kenya na Uganda.