Rais Magufuli amesema alitengua uteuzi wa Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mrisho Gambo na wenzake wawili, kutokana na kutotekeleza maagizo yake huku wakiendekeza malumbano kwa takribani miaka miwili.
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo tarehe 22 Juni 2020, wakati akiwaapisha viongozi wapya – Iddi Kimanta (Mkuu wa Mkoa wa Arusha), Kena Kihongosi (Mkuu wa Wilaya ya Arusha) na Dk. John Pima (Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha), Ikulu jijini Dar es Salaam.
Rais amesema huwa anasikitishwa sana pindi anapoona watu aliowateua kwa kuwaapisha na kuwaamini ili kufanya kazi kwa niaba ya Watanzania, wanapoenda kule hawafanyi kadri ya viapo,.
"Mtakumbuka hivi karibuni nilitengua uteuzi wa wote, sababu katika kipindi cha miaka mwili walikuwa wanagombana tu, kila mmoja ni bosi anatengeneza migogoro kwa mwenzake sikufurahishwa, walifanya kazi zao lakini waliniudhi wao kutoshirikiana na kufanya yale ambayo nimewaagiza, sasa nimewateuwa ninyi sitaki yakajitokeze hayo"-Amesema Rais Magufuli.
Aidha, rais amesema anawaamini aliowachagua viongozi hao kwa kuwa anawaamini na kuwataka wakaiendeleze miradi mbalimbali iliyopo jijini Arusha; "Kenani wewe ulikuwa Mwenyekiti wa UVCCM na ulikimbiza mwenge mwaka jana, umezunguka nchi nzima na Tanzania unaifahamu. Nina imani hauwezi kushindwa kazi Arusha"
Katika hatua nyingine, Rais Magufuli amesema amewasamehe Kamanda wa Polisi Arusha na Mkuu wa TAKUKURU mkoa huo ambao alitaka kuwafuta kazi wa kwa kile alichoeleza kuwa walifanya shughuli ambazo ziko kinyume na majukumu yao na kuwasamehe kwa sharti la kutorudia tena makosa yao, na kwamba hatosita kuwafuta kazi kama hawatabadilisha mienendo yao.