Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) taifa Dkt. John Pombe Magufuli tayari amechukua fomu ya kuwania tena nafasi ya urais.
Rais Magufuli amechukua fomu ya kugombea nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia chama chake cha CCM.
Fomu hiyo ya kuwania urais aliyoichukua amekabidhiwa na Katibu Mkuu Dkt Bashiru Ally asubuhi ya leo Juni 17,2020 jijiji Dodoma.
Akizungumza baada ya kukabidhiwa fomu hiyo, Rais Magufuli amesema ataanza mapema mchakato wa kutafuta wadhamini ili awahi kurejesha fomu hiyo ndani ya muda uliopangwa.
“Naomba nianze zoezi hili la kutafuta wadhamini, nitaenda mikoa yote kwa sababu nimekuwa nikipigiwa simu wakisema wanataka kunidhamini hivyo nitarejesha fomu yangu kwa wakati,” amesema Rais Magufuli.
Aidha, Rais Magufuli ameuthibitishia umma kuwa amekuwa akipigiwa simu na makada wa chama cha CCM ambao wamemuahidi kumdhamini katika kuwania tena kiti hicho cha urais.