Rais Magufuli ametangaza kufungua shule zote nchini na shughuli zingine za kijamii zilizokuwa zimesitishwa kutokana na ugonjwa wa COVID-19.
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo Jumanne June 16, 2020 wakati akilihutubia Bunge kabla ya kulifunga ili kupisha mchakato wa uchaguzi wa Rais, Bunge na Madiwani unaotarajiwa kufanyika Octoba Mwaka huu.
Amesema hali ya Corona nchini inaendelea vizuri na imepungua;“Kutokana na mwendendo wa corona kuendelea kuwa mzuri, corona imepungua sana, naomba nitangaze kuanzia June 29 mwaka huu nafikiri itakuwa Jumatatu, shule zote zilizokuwa zimebaki zifunguliwe, lakini Watanzania waendelee kuchukua tahadhari”.
Rais Magufuli pia ametangaza shughuli zote ambazo zilikuwa zimesitishwa kutoka na corona kurudi kama zamani, shughuli hizo ni kama kufunga ndoa ikiwa ni azma ya kuyaendeleza maisha ya zamani kuweza kurudi kama ilvyokuwa awali.
Mbali na rais Magufuli kutoa tamko hilo la ufunguzi wa shule za msingi na sekondari tarehe tajwa amewataka wananchi wote kuchukua tahadhari zilizokwishakutolewa na Wizara ya afya dhidi ya kujikinga na ugonjwa huu wa COVID-19.