Mipaka miwili ya Tanzania na Kenya eneo la Namanga na Holili imefungwa tena baada ya kuibuka hali ya sintofahamu kuhusu utekelezaji wa makubaliano yaliyowekwa kati ya nchi hizo mbili.
Madereva wa Tanzania wamelalamika kuwa vyeti vyao vimekuwa vikikataliwa wanapoingia nchini Kenya hali inayosababisha taharuki kubwa miongoni mwa madereva wa Tanzania wanaovuka mpaka wa Namanga kuingia nchini Kenya.
Mkuu wa wilaya ya Longido Frank Mwaisumbe ameeleza kuwa hakuna ushirikiano mzuri walioupata walipokuwa wakifuatialia kilichojiri katika mpaka wa Namanga.
Akiongelea adha wanayopata madereva wa malori wa Tanzania wanapoingia upande wa Kenya Mkuu huyo wa wilaya amesema suala hilo halijatolewa ufumbuzi na serikali ya Kenya ili kuondoa adha hiyo.
''Haiwezekani kwamba dereva amepimwa siku mbili tatu zilizopita kisha anarudia tena kwenda kupimwa eneo jingine kwanza tumeona kitendo hicho ni kitendo cha dharau, lakini cha pili huwezi kuvunja makubaliano bila kuwa na taarifa zozote za msingi.“ Alisema Bwana Mwaisumbe.
Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa wilaya, kwa sasa hakuna shughuli zozote zinazoendelea, mpaka wa Namanga umefungwa na kuna magari zaidi ya 500 yaliyoegeshwa Arusha, Longido na mengine Namanga.
Aidha, Madereva kutoka upande wa Kenya wamesema nchi yao hawazingatii kama Tanzania inavyozingatia; “sisi kwao wanatukubalia kutumia cheti tunachotoka nacho Kenya lakini Kenya hawakubali vyeti vya madereva wa Tanzania wakiingia upande wa Kenya hali hii inatusababisha tuumie sisi sote.'' Alisema Joseph Kariuki