Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda amesema kuwa Baraza la Mitihani ya Taifa limejiridhisha kwamba watahiniwa katika shule ya Chalinze Modern Islamic walibadilishiwa namba ya mtihani.
Kauli hii ya Waziri inakuja siku chache baada ya video zilizosambaa katika mitandao zikimuonesha mtahiniwa katika Shule ya Awali na Msingi Chalinze Modern Islamic Iptisum Suleiman Slim akilalamikia kubadilishiwa namba ya mtihani wa darasa la saba.
Prof. Mkenda amesema baada ya uchunguzi imebainika kuwa ni kweli mtahiniwa alibadilishiwa namba na kwamba pia watahiniwa wengine saba walibadilishiwa namba za mtihani.
Aidha kutokana na kukutwa na kosa hilo Serikali imeifungia shule hiyo kuwa kituo cha mitihani kwa muda usiojulikana kutokana na taarifa ya Kamati ya Mitihani ya Mkoa wa Pwani pamoja na taarifa ya Wataalamu wa Miandiko kutoka Jeshi la Polisi kubainika kuwa Watahiniwa 7 akiwemo Iptisam walibadilishiwa namba za mtihani katika Shule hiyo.
Mkenda amesema uchunguzi uliofanywa na Kamati ya Mitihani ya Mkoa wa Pwani umebaini kuwa Mtahiniwa Iptisam Suleiman Slim alifanya masomo matano kwa kutumia namba PS1408009/0040 na somo la sita (mwisho) kwa kutumia namba PS1408009/0039.