Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema serikali imeahidi kutatua changamoto mbalimbali zinazokwamisha utekelezaji wa ujenzi wa mradi mkubwa wa kiwanda cha ITRACOM FERTILIZERS LTD kitakachokuwa kinazalisha mbolea asilia ili kurahisisha usafirishaji wa malighafi pamoja na kuwa na miundombinu ya kudumu.
Amesema Serikali itasimamia ujenzi wa mradi huo ili kuhakikisha azma ya Rais Samia ya kuendeleza sekta ya kilimo inafikiwa kwa sababu changamoto kubwa iliyokuwa inawakabili wakulima wengi ni upatikanaji wa mbolea ambayo inakwenda kuwa historia.
Waziri Mkuu ameyasema hayo leo Januari 15, 2022 wakati akizungumza na uongozi na wafanyakazi wanaojenga kiwanda hicho katika eneo la Nala jijini Dodoma. “Serikali imedhamiria kuimarisha sekta ya kilimo ili Watanzania wanaoitegemea wapate mafanikio.”
Majaliwa ambaye leo alifanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi huo amesema ameridhishwa na kasi ya ujenzi wake na kwamba Serikali inataka kuona Watanzania wengi wananufaika na uwekezaji huo. Ujenzi wa kiwanda hicho umefikia asilimia 52.
“Ujenzi wa kiwanda hiki ni matokeo ya ziara ya Mheshimiwa Rais Samia nchini Burundi, lengo ni kuhakikisha tunazalisha mbolea hapa nchini badala ya kutegemea kuagiza nje kwa kiasi kikubwa. Kiwanda hiki kinatarajiwa kuzalisha tani laki 600,000 kwa mwaka,”-Majaliwa.
Kwa upande wake Waziri wa Kilimo Hussein Bashe ametoa ushauri kwa mwekezaji wa kiwanda hicho kuhakikisha anaongeza matumizi ya chokaa ili kumsaidia Mkulima kwani ardhi za baadhi ya wakulima zimechoka na njia ya kutibu tatizo hilo ni uongezwaji wa chokaa ya kutosha katika mbolea zitazozalishwa.