Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima amesema kuwa Tanzania imejiandaa kukabiliana na tishio la wimbi la nne ambalo limegundulika kuwepo kwa anuwai mpya ya kirusi kinachotambulika kwa jina la OMICRON.
Ametoa tamko la serikali dhidi ya mwenendo wa UVIKO-19 na tishio la wimbi la nne la ugonjwa huo baada ya taarifa kuenea kutoka nchi mbalimbali Duniani ambazo zimeanza kuripoti ongezeko la visa vipya vya UVIKO-19 huku ikiripotiwa kuwepo kwa tishio la kirusi kipya cha Omicron hali inayohitaji jamii kuchukia tahadhari zaidi.
Dkt. Gwajima amesema kuwa takwimu zinaonyesha hadi kufikia tarehe 29 Novemba 2021 jumla ya waliothibitika kuwa na maambukizi Duniani watu 260,867,011 kati yao vifo ni 5,200,267 ambapo takwimu za Tanzania zinaonyesha hadi kufikia Novemba 28, 2021 jumla ya watu waliothibitika kuwa na maambukizi ni 26,273 na vifo vilivyotokea ni 731 ambavyo vimetolewa taarifa.
Aidha, amesema kuwa jukumu la kinga dhidi ya magonjwa yote ni la kila mwananchi ambapo Serikali kupitia Wizara ya Afya na wadau wake kwa pamoja wanasimamia utekelezaji wa afua mbalimbali ili kuwezesha jamii kujikinga na UVIKO-19 wakati serikali ikiwezesha upatikanaji wa chanjo.
Dkt. Gwajima amesema kuwa serikali imepokea chanjo ya Jansen dozi 1,227,400, Sinopharm dozi 2,578,400 na chanjo aina Pfizer hadi kufikia 28 Novemba 2021 jumla ya wananchi waliopata chanjo 1,520,275 sawa na asilimia 2.7 ya watanzania Wote.