Rais Samia Suluhu Hassan amewataka viongozi wa serikali za mitaa kutoa elimu ya kutosha juu ya umuhimu wa chanjo ya UVIKO-19 kwa wananchi.
Rais Samia Suluhu Hassan amewataka viongozi hao kutotumia mabavu katika utoaji wa chanjo bali kuwaelimisha wananchi wapate chanjo kwa hiari.
Rais ametoa kauli hiyo leo wakati akifungua mkutano mkuu maalum wa uchaguzi wa viongozi wa jumuiya ya serikali za mitaa ALAT Taifa Mkoani Dodoma.
“Tulisema hili jambo ni la hiari, ukipita nyumba kwa nyumba anayetaka mchome asiyetaka usichome Lakini kubwa ninalotaka kusema mtu ana hiyari ya kukubali au kukataa na kama ana elimu ya kutosha, hawezi kukataa”-Rais Samia Suluhu Hassan
Katika mkutano huo maalum Rais Samia Suluhu Hassan amewataka viongozi hao kushirikiana na kuondoa tofauti Zao ambazo nyingi hutokana na maslahi binafsi.
Aidha, Rais Samia amewakumbusha viongozi hao kuhakikisha wanawatumikia wananchi vema kwa kutatua changamoto zao na si vinginevyo.
"Katika mkutano mmoja nilisema sitaki kuona mabango yenye masikitiko, yenye shukrani wacha wananchi waandike, mabango yenye masikitiko ni kwa sababu viongozi kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa hamfanyi kazi yenu, baadhi yenu ni sehemu ya kero".
Rais Samia Suluhu Hassan leo Septemba 27, ameshiriki mkutano mkuu maalum wa uchaguzi wa viongozi wa jumuiya ya tawala za mitaa tanzania (ALAT) katika ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Center Jijini Dodoma.