Rais Samia Suluhu Hassan amewataka viongozi wa dini kuendelea kuwasisitiza waumini kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa COVID-19 unaosababishwa na virusi vya corona.
Rais Samia ametoa wito huo wakati akizungumza na Baraza la Maaskofu Wakatoliki Tanzania jijini Dar es Salaam na kuthibitisha kwamba kuna viashiria vya wimbi la tatu la virusi vya Corona nchini.
"Msisahau kuwakumbusha na kuwahimiza waumini kuhusu umuhimu wa kujikinga na kuchukua tahadhari zote zinazoelekezwa na watalaamu wa afya dhidi ya ugonjwa wa corona kwa kuwa kinga ni bora kuliko tiba, tusiache kutumia kila kitakachotukinga na maradhi haya ili kuepusha vifo vya makundi, kama tunavyojua duniani sasahivi kuna wimbi la tatu la corona, tumetoka kwenye wimbi la kwanza......tumeingia wimbi la pili na sasa kuna wimbi la tatu"-Rais Samia.
Aidha, Rais Samia amewasihi viongozi wa dini kuendelea pia kumtanguliza Mwenyezi Mungu wakati wakichukua tahadhari za ugonjwa COVID-19.
"Ishara ndani ya nchi zimeanza kuonekana, tayari tuna wagonjwa ambao wameshaonekana katika wimbi hili la tatu la corona, kama mnakumbuka siku nilitembelea hospitali ya Mwananyamala kuna wodi daktari mfawidhi alikuwa ananiingiza akaniambia humu kuna wagonjwa wenye matatizo ya kupumua, nikamwambia hebu kuwa muwazi ni 'COVID' akaniambia ndio ni 'COVID' wakati wapiga picha wangu walikuwa wameshatangulia nikawaambia nyinyi tokeni haraka huko, kwahiyo ni kusema kwamba hili jambo bado lipo tuchukue tahadhari zote na ni vema tumuombe Mungu aendelee kutuepusha"-Rais Samia.
Kwa upande wake Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Gervas Nyaisonga amempongeza Rais Samia kwa kuendelea kuboresha sekta mbalimbali hususani anavyoshirikiana na taasisi za dini katika kutoa huduma za kijamii hapa nchini.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameendelea na adhma yake ya kukutana na kuzungumza na makundi maalum, Ambapo Juni 15 alikutana na vijana jijini Mwanza, Leo Juni 25 na amezungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Kurasini-Temeke Dar es Salaam.