Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema Sekta ya Sanaa, Utamaduni na Michezo inakua kwa kasi kubwa na inatoa fursa ya ajira kwa vijana nchini.
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Jijini Dodoma wakati anahutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutoa mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Sita ikiwa ni utamaduni wa Rais kuhutubia Bunge baada ya kuapishwa kushika madaraka hayo.
“Vijana wetu wengi wamepata ajira kupitia sekta hii, hivyo basi kama ilivyoahidiwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020, kwenye miaka hii mitano tunakusudia kuikuza zaidi sekta hii hususani kwa kuimarisha usimamizi wa masuala ya Hati Miliki ili wasanii waweze kunufaika na zao” amesema Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Kuhusu Mfuko wa Utamaduni na Sanaa, Rais amesema Serikali kusimamia na kuhuisha Mfuko huo ili kuwasidia wasanii nchini kupata mafunzo na mikopo ambayo itasaidia kukuza uchumi wao na taifa kwa ujumla.
Aidha, Rais ameongeza Serikali imeanza kutenga fedha kidogo kidogo kwa ajili ya timu za Taifa zikiwemo za wanawake lengo ni kuhakikisha sekta hiyo inapata msukumo na ari za wachezaji ili Tanzania iweze kuingia kwenye ramani ya mchezo wa soka.
Rais Samia wakati akilihutubia aliliambia bunge kuwa serikali itafanya mabadiliko ya kisera na sheria ili kuwavutia wawekezaji zaidi nchini.
Amesema kwa kuwa kumekuwa na malalamiko juu ya urasimu, na kutokutabilika kwa sera za uwekezaji, eneo hilo litawekewa kipaumbele ili kutoa tija kwa uchumi wa taifa hilo.
Rais Samia pia amesema serikali itaendelea kulilea shirika la nchi la ndege la ATCL kimkakati ikiwemu kulitua mzigo wa madeni
"Hatutakubali liendelee kutengeneza hasara baada ya uwekezaji mkubwa uliofanyika...Tunaenda kulifanyia uchambuzi yakinifu na tutawaweka watua ambao wataliongoza ili kutengeneza faida."
KAtika hotuba ya Rais iliyokuwa imesheheni mambo mengi, Rais Samia pia hakusahau kuzungumzia habari za uchonganishi zinazoendelea katika mitandao ya kijamii.
"Taarifa tuliyopewa juu ya kifo cha mpendwa wetu ni udhaifu wa moyo ambao ameishi nayo kwa zaidi ya miaka kumi. Nimekuwa nikifuatilia mitandao ya kijamii, kuna watu huko mitandaoni wanasema, fulani na fulani wamempa sumu. Habari hizi zinaleta uchonganishi wa koo na koo, makabila na makabila, Kama wana taarifa waje tuwasikilize na taarifa zao." ameeleza Rais Samia.
Amewataka watu wanaotumia mitandao ya kijamii kufanya uchonganishi kuacha tabia hiyo na kurudi kwa Mwenyezi Mungu kwa kujiuliza kama mambo ya uchonganishi wanayotenda ni sahihi.
Rais Samia Suluhu Hassan kwa mara ya kwanza amelihutubia bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tangu alipoapishwa Machi 19, 2021 kuwa Rais wa Tanzania.