Mkuu wa Wilaya ya Mjini visiwani Zanzibar, Rashid Msaraka ametangaza kuanza operesheni ya kuwanyoa nywele vijana wenye umri chini ya miaka 18, waliofuga rasta au kunyoa mtindo wa panki.
Bwana Rashid amesema kama vijana hao wanataka kufuga rasta hizo wakafugie sehemu nyingine na endapo wazazi wao wameshindwa kuwakata hizo nywele, atawakata yeye.
''Vijana wote wenye umri chini ya miaka 18 kama huyu..kama wazee wao wameshindwa kuwakata hizi nywele tutawakata sisi'' alitahadharisha kiongozi huyo.
Aidha, picha ya video imesambaa katika mitandao ya kijamii ikionesha msaidizi wa kiongozi huyo akimkata nywele kijana aliyekuwa amezisokota nywele zake.
Kitendo hicho kimeibua mjadala kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii, watu wakihoji ni sheria ipi iliyomuongoza kiongozi huyo kutoa agizo la kumkata nywele kijana huyo.