Mgombea urais wa JMT kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Tundu Lissu amezitaka Jumuiya za Kimataifa pamoja na jumuiya za kikanda ziingilie kati taarifa za matokeo ya uchaguzi wa Tanzania.
Lissu amesema hayo wakati akizungumza na Waandishi wa Habari leo Oktoba 29,2020 ambapo ameeleza kuwa Jumuiya za Kimatifa zitoe taarifa za ukweli na Watanzania waingilie kudai haki yao kwa amani kwa njia ya kidemokrasia.
Aidha, Lissu amesema kuwa chama chake kimeweka wagombea 244 wa ubunge nchi nzima, kati ya hao 63 walienguliwa, udiwani 3754 kati yao wagombea 1025 walienguliwa, hivyo takribani 30% walienguliwa.
Mgombea Urais huyo amedai kuwa mawakala wengi wa upinzania hawakupewa barua ya kuingia kwenye vituo vya kupigia kura; "Mawakala waliobaki kwenye vituo hakuna aliyepewa nakala ya matokeo ya uchaguzi kama sheria inavyotaka,hiyo peke yake inathibitisha hakuna uchaguzi wa vyama vingi, hata kwa sheria zetu kama zilivyo huu haukua uchaguzi majimbo yote , kata zote CCM wametangaza ushindi".
Aidha, wakati hayo yakiendelea kubainishwa na Lissu, Tume ya Taifa ya Uchaguzi Tanzania imekanusha madai hayo ya upinzani na kusema tuhuma zinazotolewa hazijawasilishwa rasmi.