Kiongozi wa Kazakhstan anayeiongoza nchi hiyo kimabnavu anasema ameidhinisha vikosi vya usalama "kufyatua risasi bila onyo" huku kukiwa na msako mkali dhidi ya maandamano dhidi ya serikali.
Rais Kassym-Jomart Tokayev pia alisema "majambazi 20,000" wameshambulia mji mkuu wa Almaty, kitovu cha maandamano yaliyochochewa na ongezeko la bei ya mafuta.
Wizara ya mambo ya ndani inasema "wahalifu wenye silaha" 26 na maafisa wa usalama 18 wameuawa kufikia sasa katika machafuko hayo.
Katika hotuba yake kwa njia ya televisheni, Bw Tokayev alisema vikosi vya kulinda amani vilivyotumwa kutoka Urusi na mataifa jirani vimefika kwa ombi lake na viko nchini kwa muda ili kuhakikisha usalama.
Kikosi kutoka kwa Jumuiya ya Mkataba wa Usalama wa Pamoja (CSTO) inayoongozwa na Urusi inaripotiwa kuwa na wanajeshi 2,500. Bw Tokayev alitoa "shukrani maalum" kwa Rais wa Urusi Vladimir Putin kwa kutuma wanajeshi.
Mapema siku ya Ijumaa, milio mipya ya risasi ilisikika karibu na uwanja mkuu wa Almaty.