Gavana wa jimbo la Florida nchini Marekani ambaye ni wa chama cha republican Ron DeSantis amesaini sheria ya kuzuia michezo ya wasichana waliobadili jinsia ambapo amesema kwamba ni muhimu maadili ya mashindano ya shule za umma yakalindwa.
Florida limekuwa jimbo la kwanza mwaka huu kupiga marufuku wanawake na wasichana waliobadili jinsia zao kushiriki michezo katika shule za umma ya kike.
Gavana wa jimbo hilo Mrepublican, Ron DeSantis amesaini sheria ya marufuku hiyo siku ya Jumanne.
Sheria hiyo inasema wanawake na wasichana wanapaswa kucheza katika timu za jinsia ya kibaiolojia iliyoandikwa kwenye cheti chao cha kuzaliwa.
Wanaharakati kutoka makundi ya wapenzi wa jinsia moja, na waliobadili jinsia - LGBT wamepinga hatua hiyo ambayo wameitaja kama ya ubaguzi huku kundi moja kikiapa kupinga sheria hiyo kisheria.
"Tunaamini kwamba ni muhimu kwamba maadili ya mashindano haya yanapaswa kulindwa, Tutaenda kwa misingi ya kibaiolojia, sio kwa misingi ya itikadi wakati tunapofanya michezo."- Bw. DeSantis alisema alipokuwa akisaini sheria hiyo katika Shule ya Kikristo iliyopo katika mji wa Jacksonville.
Mwakilishi wa jimbo la Florida Carlos Smith, kutokea chama cha democratic ambaye anatambuliwa kama Latino na anayeshiriki mapenzi ya jinsia moja, alipinga muswada huo ambao ameutaja kama wa kutisha.
"Hii inachochea chuki dhidi ya waliobadili jinsia na kuwaweka watoto hatarini bila sababu yoyote,"-aliandika Smith kwenye Twitter.
#Chanzo:BBCSwahili