Mizinga 41 ya heshima ilipigwa leo Aprili 10 nchini Uingereza, rasi ya Gibraltar na kwenye meli zote za jeshi la nchi hiyo kumkumbuka mume wa Malkia Elizabeth wa Pili, Mwanamfalme Philip aliyeaga dunia jana Ijumaa.
Heshima hiyo ya kijeshi ilitolewa majira ya mchana siku moja tangu ilipotangazwa kuwa Mwanamfalme Phillip amefariki dunia akiwa kwenye kasri wa Windsor baada ya kuugua kwa wiki kadhaa.
Salamu za rambirambi zimeendelea kutolewa kutoka kila pembe ya dunia kukumbuka maisha ya Mwanamfalme Phillip ambaye amekuwa mume na nguzo muhimu katika utawala wa Malkia Elizabeth kwa zaidi ya miaka 70.
Katika salamu zake za pole, kiongozi wa kanisa katoliki duniani Papa Francis amemwelezea mwanamfalme Philip kuwa mtu aliyejitolea kwa ajili ya familia yake na kuwa na mchango mkubwa katika sekta ya elimu.
Mwanamfalme Philip atazikwa kwa heshima zote za kifalme lakini mazishi yake yanapangwa kufanyika kwa taratibu tafauti kutokana na vizuizi vya kupambana na janga la virusi vya corona.