Mwanamfalme Philip ambaye ni mume wa Malkia Elizabeth II wa Uingereza amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 99, Kasri la Buckingham limetangaza.
Tangazo kutoka Kasri ya Buckingham limeeleza kuwa: "Ni kwa masikitiko makubwa, Malkia ametangaza kifo cha mumewe mpenzi, Mwanamfalme Philip, Duke (Mtawala) wa Edinburgh".
Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson anasema ni kwa huzuni kubwa kupokea habari za kifo cha Mwanamfalme Philip kutoka Kasri la Buckingham.
Akitoa salamu zake za rambirambi alisema Mwanamfalme Philip alipata mapenzi ya vizazi nchini Uingereza, katika Jumuiya ya Madola na ulimwenguni kote
"Alikuwa mshirika wa kifalme aliyehudumu kwa muda mrefu katika historia, mmoja wa watu wa mwisho nchi hii kuwahi kutumika katika Vita vya pili vya na alitajwa katika barua za ushujaa."
Katika rambirambi zake, Boris Johnson alisema, "alisaidia kuongoza familia ya kifalme na ufalme ili iweze kuwa taasisi muhimu bila shaka kwa usawa na furaha ya maisha yetu ya kitaifa."
Waziri mkuu anamnukuu Malkia wakati mmoja akisema nchi hiyo inadaiwa na mumewe deni kubwa kuliko "tunavyopaswa kujua", na kuongeza kuwa alikuwa na hakika kuwa makadirio hayo yalikuwa sahihi.
"Tunaomboleza leo na Malkia, tunampa pole zetu, na familia yake yote na tunashukuru, kama taifa na ufalme, kwa maisha ya kipekee na kazi ya Mwamfalme Philip, Mtawala wa Edinburgh,"- alisema.
Mwanamfalme Philip alimuoa Binti mfalme Elizabeth mnamo 1947, miaka mitano kabla ya kuwa Malkia, na amekuwa mwenza wa mfalme ama malkia aliyehudumu kwa muda mrefu zaidi katika historia ya Uingereza.