Waziri wa Afya Prof. Jean Louis Rakotovao wa Madagascar amesema taifa lake limekubali kupata chanjo ya ugonjwa wa COVID-19.
Taifa hilo limeamua kubadili mtazamo wake juu ya kukabiliana na virusi vya corona na kujumuika na jitihada za kimataifa kupata chanjo ya corona ambazo zimethibitishwa na Shirika la Afya Duniani.
"Kuna hatua kadhaa ambazo inabidi kupitia kabla ya kupata chanjo hiyo lakini kujisajili ndio jambo la msingi na hatua muhimu kabla ya kupata chanjo hiyo, lakini tayari tuko kwenye hatua muhimu katika usajili," - Waziri wa Afya Prof Jean Louis Rakotovao amesema kwenye video aliyoiweka kwenye ukurasa wa Wizara yake wa Facebook.
Awali Madagascar ilionesha kutokuwa na nia ya kushiriki katika jitihada za kupokea chanjo. Ilidai kuwa ni bora kutumia dawa ya asili inayofahamika kama Covid-Organics.
Dawa hiyo ambayo iko katika mfumo wa chai au vidonge ilitangazwa na Rais wa taifa hilo bwana Andry Rajoelina kuwa ndio dawa ya corona.
Aidha, Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani hakuna tiba ya virusi vya corona iliyopatikana mpaka sasa.