Kiongozi wa kanisa katoliki duniani Papa Francis, amekamilisha ziara yake ya kihistoria nchini Iraq, iliyokuwa na nia ya kuleta matumaini katika taifa hilo lililo na wakristo wachache akiwa na ujumbe wa mshikamano, amani na kusameheana.
Katika ziara yake ya siku nne Papa aliye na umri wa miaka 84 alitembelea mikoa mitano nchini Iraq.
Katika kila eneo alilolitembelea, Papa alitoa ujumbe wa umoja kuanzia Najaf Kusini mwa taifa hilo alikokuwa na mkutano wa kihistoria na kiongozi wa waislamu wa madhehebu ya Shia, Ayatollah Ali al-Sistani hadi katika eneo la Nineveh.
Kiongozi huyo wa Kanisa Katoliki alikutana na kusikiliza masaibu ya waathiriwa waliopitia mateso chini ya kundi la wanamgambo wanaojiita dola la kiislamu.
Sehemu kubwa ujumbe wa Papa Francis kwenye zaira nchini Iraq ni kutoa wito wa amani na msamaha hasa kwa jamii za wakristo wanaolengwa na wapiganaji wa itikadi kali.
Aidha, Inakadiriwa kulikuwa na zaidi ya wakrsito Milioni 01 nchini Iraq lakini idadi yao imepungua na kufikia kati ya 250,000 hadi 400,000 baada ya miongo kadhaa ya vita, unyanyasaji wa kidini na hali ngumu ya uchumi.
Vatican inatumai ziara ya Baba Mtakatifu ambayo ni ya kwanza kufanya na kiongozi wa kanisa katoliki itafufua matumaini ya wakristo wa Iraq.