Kiongozi wa upinzani nchini Ethiopia Jawar Mohammed, sambamba na watu wengine 19, wamekuwa kwenye mgomo wa kutokula kwa zaidi ya siku 13, kwa mujibu wa mawakili wao.
Kundi hilo lilishtakiwa kwa kujihusisha na vitendo vya kigaidi kuhusiana na wimbi la vurugu za wenyewe kwa wenyewe baada ya kuuawa kwa mwanamuziki maarufu nchini humo, Hachalu Hundessa.
Zaidi ya watu 150 walipoteza maisha wakati wa vurugu hizo baada ya mtumbuizaji huyo kutoka kabila la Oromo kupigwa risasi mjini Addis Ababa.
Bw. Jawar na Bekele Gerba, Naibu Mwenyekiti wa chama cha Oromo Federalist Congress (OFC) ni miongoni mwa waliokuwa kwenye mgomo wa kutokula katika gereza la Kallitti.
Wanataka ''kuachiliwa kwa wafungwa wote wa kisiasa wa kabila la Oromo na kukoma kwa uonevu wa familia za wafungwa wa kisiasa'', mawakili waliandika kwenye ukurasa wa Facebook.
Mmoja wa mawakili, Kedir Bulo, aliiambia BBC idhaa ya Afaan Oromoo kuwa wafungwa wanne walizirai siku chache zilizopita na baadhi walikimbizwa hospitalini kwa ajili ya matibabu zaidi.
Mamlaka hazijasema chochote kuhusu mgomo wa kutokula.
Familia zilizozungumza na BBC zimesema kuwa walikuwa na hofu kuhusu hali za wafungwa
Aidha, Siku ya Jumanne makundi ya kidini na viongozi wa kisiasa walijaribu kuwashawishi wafungwa kumaliza mgomo bila mafanikio.