Mwanachama wa Republican anasema kwamba atakuwa Seneta wa kwanza kupinga kuidhinishwa kwa Joe Biden kama Rais wa Marekani wakati bunge la Congress litakapomuidhinisha rais huyo mteule wiki ijayo.
Seneta wa Missouri Josh Hawley alisema kwamba alikuwa na wasiwasi wa maadili licha ya kutokuwa na ushahidi wa kuwepo kwa udanganyifu katika uchaguzi uliopita.
Kundi moja la wanachama wa Republican katika bunge la wawakilishi pia linapanga kupinga matokeo ya uchaguzi.
Baraza la wajumbe linaloidhinisha matokeo ya uchaguzi kwa kutoa pointi kwa kila jimbo lililoshindwa na wapinzani hao wawili mapema liliidhinisha ushindi wa rais mteule Joe Biden dhidi ya Trump kwa 306-232,.
Kura hizo ni lazima zihakikiwe na bunge la Congress ifikiapo Januari 6, Ambapo siku ya kuapishwa kwa Rais huyo mteule na Makamu wake itakuwa tarehe Januari 20,2021.
Tangu aliposhindwa katika uchaguzi, bwana Trump mara kadhaa amedai kwamba kulikuwa na udanganyifu wakati wa shughuli hiyo bila ya kutoa ushahidi.
Hatua za kisheria za Rais huyo wa chama cha Republican kubadilisha matokeo zimekataliwa na mahakama.
Bwana Hawley alisema hangeweza kupiga kura ili kuidhinisha matokeo hayo bila kusema wazi kwamba baadhi ya majimbo hususani Pennsylvania, lilishindwa kuheshimu sheria zake za uchaguzi.
Alisema kwamba bunge la Congress linapaswa kuchunguza madai ya udanganyifu wa kura na kuchukua hatua zitakazolinda maadili ya uchaguzi.
Bwana Hawley ambaye ni seneta kwa mara ya kwanza anyeidaiwa kuwa na hamu ya kuwania urais hakutoa ushahidi wowote ambao huenda ungebadilisha matokeo rasmi.