Watawala wa kijeshi wa Sudan na viongozi wa vuguvugu la maandamano wamekubaliana juu ya kuundwa kwa utawala wa mpito wa miaka mitatu, ambao utakabidhi madaraka kamili kwa raia.
Mjumbe wa baraza la kijeshi linaloongoza nchi hiyo, Luteni Jenerali Yasser al-Atta ametangaza muafaka huo muda mfupi uliopita mbele ya waandishi wa habari. Al-Atta amesema makubaliano ya mwisho ya kugawana madaraka, na kuundwa kwa taasisi za uongozi wa mpito yatatiwa saini baina ya wanajeshi na waandamanaji katika muda usiozidi saa 24, chini ya masharti yanayokidhi matakwa ya umma wa Sudan. Afisa huyo amesema miezi sita ya kwanza itatengwa maalum kufikia makubaliano ya amani na makundi ya waasi ndani ya nchi hiyo. Amesema pia kuwa bunge la mpito litakuwa na viti 300, asilimia 67 ya viti hivyo ikikaliwa na wanachama wa vuguvugu la waandamanaji lijulikanalo kama ''Muungano kwa ajili ya Uhuru na Mabadiliko''.
CHANZO: Idhaa ya Kiswahili DW