Watawala wa kijeshi wa Sudan na viongozi wa maandamano wameanza tena leo mazungumzo juu ya kukabidhi madaraka kwa serikali ya kiraia baada ya siku kadhaa za mkwamo katika majadiliano. Viongozi wa maandamano Omar al-Digeir na Satea al-Haj ni miongoni mwa wanaohudhuria mazungumzo hayo kwa niaba ya vuguvugu la Allance for Freedom and Change.
Mkutano huo wa faragha unaandaliwa katika jumba la mikutano katikati ya mji mkuu Khartoum. Duru hii mpya ya mazungumzo imekuja wakati maelfu ya waandamanaji wakiendelea kupiga kambi nje ya makao makuu ya jeshi katikati ya Khartoum. Makamanda wa kijeshi na waandamanaji wanatofautiana kuhusu ni nani atakayeshirikishwa katika serikali ya mpito itakayochukua nafasi ya baraza la sasa la kijeshi. Wakuu wa jeshi wanapendekeza kuwa baraza jipya la mpito liongozwe na jeshi, wakati viongozi wa maandamano wanataka liendeshwe kwa kiasi kikubwa na raia.
CHANZO: Idhaa ya Kiswahili DW