Vifaru 24 wameuawa nchini Afrika Kusini katika takriban wiki mbili, wizara ya mazingira imethibitisha.
Maamlaka nchini humo zinasema mizoga saba ilipatikana katika Hifadhi ya Kitaifa ya Kruger, mingine saba katika jimbo la Mpumalanga, sita KwaZulu-Natal na minne Cape Magharibi.
Wizara hiyo imelaani kuendelea kwa ujangili na mauaji ya vifaru kwa ajili ya pembe zao, ikisema washukiwa tisa wa uhalifu huo wamekamatwa katika siku 14 za kwanza za mwezi wa Disemba.
Imewahimiza wananchi kusaidia kwa taarifa zozote zinazoweza kusababisha kukamatwa na kufunguliwa mashtaka kwa majangili.
Afrika Kusini ni makao ya karibu 80% ya idadi ya vifaru barani Afrika, ambayo iko chini ya 30,000.
Mamia huuawa kila mwaka kwa ajili ya pembe zao, nyingi kati yao zikielekea Asia ambako pembe za faru ni kiungo katika dawa na tiba asilia.
Idara ya mazingira inasema itatoa taarifa kuhusu jumla ya idadi ya vifaru waliouawa kwa ajili ya pembe zao mwaka wa 2021 mapema mwaka wa 2022.